Malaria kutokomezwa ifikapo mwaka 2050?;

Dunia inaweza kutokomeza kabisa malaria- moja kati ya magonjwa hatari yanayoathiri binaadamu- ripoti imeeleza.

Kila mwaka kuna zaidi ya watu milioni 200 wanaougua ugonjwa huu, hasa ukiua watoto wadogo.

Ripoti inasema kutokomeza malaria si ndoto, lakini kupambana na vijidudu pengine kutahitaji dola bilioni 2 kama ziada kwa mwaka.

Malaria ni nini?

Malaria ni ugonjwa unaosababishwa na vijidudu kitaalamu viitwavyo Plasmodium

Husambaa kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine baada ya kuumwa na mbu jike wanaokuwa wakitafuta damu kwa ajili ya chakula.

Mtu anapoumwa huugua homa kali.

Vijidudu hivyo huathiri seli kwenye ini na chembechembe nyekundu za damu, na kusababisha dalili nyingine ikiwemo upungufu wa damu.

Hatimaye ugonjwa huathiri mwili mzima, ikiwemo ubongo na unaweza kuua.

Takriban watu 435,000- wengi wao watoto- hufa kutokana na malaria kila mwaka.

Hali ikoje hivi sasa?

Dunia imepiga hatua kubwa tayari katika kupambana na malaria.

Tangu mwaka 2000:

Idadi ya nchi zinazokabiliwa na ugonjwa huu imepungua kutoka 106 mpaka 86.Idadi ya watu wanaougua malari imepungua kwa asilimia 36Idadi ya vifo imeshuka kwa asilimia 60

Hii inatokana na kutumia njia mbalimbali za kuzuia mbu kama vile neti zenye dawa na dawa za kutibu watu wanaougua malaria.

Kwanini ripoti hii ni muhimu?

Kutokomeza malaria- Kutokomeza ugonjwa huu duniani -kutakuwa mafanikio makubwa sana.

Ripoti ilitolewa na shirika la afya duniani WHO miaka mitatu iliyopita kutathimini kwa namna gani itawezekana kutokomeza ugonjwa huu na gharama itakayotumika.

Wataalamu 41 duniani- wanasayansi na wachumi wamehitimisha kwa makadirio kuwa ugonjwa huu utatokomezwa kabisa ifikapo mwaka 2050.

Ripoti yao, iliyochapishwa na jarida la kitabibu la Lancet imeelezwa ripoti hiyo kuwa ''ya kwanza na ya aina yake''.

''Kwa muda mrefu imekuwa ikionekana kuwa kutokomeza malaria ni kama ndoto, lakini sasa tuna ushahidi kuwa malaria inaweza na inapaswa kuwa imetokomezwa kabisa ifikapo mwaka 2050,'' alisema mtaalamu Richard Feachem, mmoja kati ya waandishi wa ripoti.

''Ripoti hii inaonesha kuwa kutokomeza ugonjwa wa malaria miongoni mwa jamii inawezekana.''

Hatahivyo, ametahadharisha kuwa ''zinahitajika juhudi kubwa'' kufikia lengo hilo.

Ripoti inakadiria kuwa, dunia itakuwa imetokomeza malaria ''kwa kiasi kikubwa'' kabisa ifikapo mwaka 2050.

Lakini kutakuwa na maeneo kadahaa barani Afrika, kuanzia Senegal kaskazini magharibi mpaka Msumbiji kusini mashariki.

Kuondokana na ugonjwa wa malaria kunahitaji teknolojia kutumika ipasavyo, na kutumika kwa njia mpya za kupambana na ugonjwa wa malaria, ripoti imeeleza.

Njia hizo inahusisha pia kuwafanya mbu wasizaliane na kuleta athari kwa binaadamu.

Mfalme mswati wa tatu wa Eswatini (zamani Swaziland) na mwenyekiti wa viongozi wa Afrika walio mstari wa mbele kwenye mapambano dhidi ya malaria amesema: ''kutokomeza malaria ni jambo linalowezekana na la muhimu. ''Lazima tuhakikishe kuwa uvumbuzi ni jambo linalopewa kipaumbele''.

Itagharimu kiasi gani?

Ripoti inakadiria kuwa pauni bilioni 3.5 hutumika kila mwaka kwa wakati huu.

Lakini ziada ya dola bilioni 2 kwa mwaka inahitajika kuondokana na ugonjwa huu ifikapo mwaka 2050.

Waandishi wa ripoti wanasema kumekuwa na gharama kutokana na watu kupoteza maisha na mapambano dhidi ya vijidudu vinavyosababisha malaria pia kupambana na mbu.


 Malaria itatokomezwa ifikapo 2050?

Kutokomeza ugonjwa huu ni changamoto duniani kote.

Iliwahi kufanyika mara moja pekee- surua ilipotangazwa kutokomezwa kabisa mwaka 1980.

Ilihitajika nguvu kubwa na chanjo madhubuti kupambana na ugonjwa huo.

Lakini kuna sababu ya kwanini surua ni ugonjwa pekee, na historia ya virusi vinavyosababisha polio inaonyesha jinsi gani mchakato huu wa kutokomeza ugonjwa ulivyo na changamoto nyingi.

Kuna maoni gani?

''Kutokomeza malaria umekuwa mpango wa karne, na inathibitisha kuwa ni mpango wenye changamoto,'' anasema Daktari Tedros Ghebreyesus, mkurugenzi mkuu wa WHO.

''Lakini hatuwezi kufikia malengo ndani ya kipindi hiki kwa zana na mbinu zilizopo hivi sasa-mbinu ambazo zilibuniwa karne iliyopita au hata zaidi.''

Daktari Fred Binka wa chuo kikuu cha sayansi shirikishi nchini Ghana, anasema: ''kutokomeza malaria kunahitaji malengo, kujitoa na kushirikiana na wengine zaidi kuliko ilivyokuwa awali, tukijua kuwa faida yake si kuwa itaokoa maisha ya watu bali pia itaimarisha uchumi wa dunia''.

.


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Umoja wa Ulaya hatimaye wakubaliana kuufufua uchumi wao

Urusi kuisadia Uganda kujenga uwezo wake wa nyuklia, ni mataifa gani ya Afrika yanatumia nishati ya nyuklia na kwanini?