Virusi vya corona: Kwanini dunia inaitegemea India kutengeneza chanjo ya virusi hivi?

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo wiki mbili zilizopita alisema kuwa India na Marekani zinafanya Kazi pamoja kutengeneza chanjo ya kukabiliana na virus vya corona
Tamko la Bw. Pompeo halikuwa la kushangaza kwani nchi hizo mbili zishawahi kushirikiana katika mpango wa kutengeza pamoja chanjo iliyotambulika kimataifa kwa zaidi ya miongo mitatu.
Wamefanya kazi pamoja katika juhudi za kukomesha homa ya dengue, magonjwa ya enteric, influenza na kifua kikuu. Majaribio ya chanjo ya dengue yamepangwa kufanyika hivi karibuni.
India ni miongoni mwa watengenezaji wakuu wa dawa mbadala na chanjo duniani.
Nchi hiyo inasifika kwa kutengeza chanjo maarufu na zingine ndogo, kutengeza dozi ya chanjo dhidi ya polio, utandu wa ubongo, homa ya mapafu, rotavirus, BCG, ukambi na rubella, miongoni mwa magonjwa mengine.
Kwa sasa nusu ya mashirika ya India yako mbioni kutengeza chanjo dhidi ya virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Covid-19.
Moja ya mashirika hayo ni Taasisi ya Serum nchini India, watengenezaji wakuu wa chanjo duniani kulingana na idadi ya dozi ya chanjo walizotengeneza na kuuza kimataifa.
Kampuni hiyo ya miaka 53 hutengeza dozi bilioni 1.5 ya chanjo kila mwaka, kutoka kwa viwanda vyake viwili yalivyopo katika mji wa magharibi Pune. (Ina viwanda vingine vidogo nchini Uholanzi na Jamhuri ya Czech.) Karibu watu 7,000 wanafanya kazi katika kampuni hiyo.
Kampuni hiyo inasambaza karibu chanjo 20 katika jumla ya mataifa 165. Asilimia 80 ya chanjo zake zinasafirishwa nje ya nchi kwa gharama ya senti 50 kwa dozi, ambayo inakadiriwa kuwa bei rahisi zaidi duniani.
Sasa kampuni hiyo inashirikiana na Codagenix, ambayo ni kampuni ya utengenezaji madawa ya Marekani kutengeneza asilimia 80 ya chanjo zote duniani.
Chanjo hii hutengezwa kupunguza makali ya virusi- Ama kukabiliana na viini hatari - ndani ya pathogen ambazo hazisababishi magonjwa. (Kwasababu zimedhoofishwa katika mazingira ya maabara.)
"Tunapanga kufanya majaribio ya chanjo hii kwa wanyama [panya na sokwe] Aprili. Kufikia Septemba, tutaanza kufanya majaribio kwa binadamu," Adar Poonawalla, Afisa mkuu mtendaji wa Taasisi ya Serum nchini India, aliambia Newsday Swahili kwa njia ya simu.
Kampuni ya Bw. Poonawalla pia imeshirikiana na Chuo kikuu cha Oxford kutengeneza chanjo ambayo inaungwa mkono na serikali ya Ungereza.
Majaribio ya chanjo hiyo katika chuo kikuu cha Oxford kwa binadamu yalianza kufanywa Alhamisi iliyopita.
Kila kite kikienda sawa, wanasayansi wanalenga kutengeneza angalau dozi milioni moja kufikia mwezi Septemba.
"Ni wazi kwamba ulimwengu utahitaji mamilioni ya chanjo, ikiwezekana kufikia mwisho wa mwaka huu, ili kukomesha janga hili lililosababisha mataifa kuweka amri ya kutotoka nje," Prof Adrian Hill, ambaye anaendesha Taasisi ya Jenner mini Oxford, aliiambia Newsday Swahili
Ni hapa ambapo watengenezaji chanjo wa India. Kampuni ya Bw.Poonawalla pekee ina uwezo wa kutengeza kati ya dozi milioni 400 hadi 500 million. "Tuna uwezo mkubwa kwasababu tumewekeza katika nyanja hii," alisema.
Kuna zingine kadhaa. Kampuni ya utengezaji dawa ya Bharat liyopo mjini Hyderabad ilitangaza ushirikiano wake na Chuo Kikuu cha Wisconsin Madison na kampuni ya Marekani ya FluGen kutengeza karibu dozi milioni 300 ya chanjo itakayosambazwa duniani.
Zydus Cadilla inafanyia Kazi chanjo mbili, huku Biological E, Indian Immunologicals, na Mynvax zote zikifanyia kazi chanjo moja kila moja. Chanjo zingine kama nne ama tano zilizotengezwa nchini humo zipo katika awamu ya kwanza ya utengenezaji wake.
"Shukurani za dhati ziendee makampuni ya kutengeneza dawa ambayo yamewekeza katika mchakato mzima wa kuhakikisha chanjo zinatengezwa kwa wingi. Wamiliki wa kampuni hizi pia wana lengo kuhudumia ulimwengu, na wakati huo huo kuendesha biashara zilizostawi kwa manufaa ya watu wote," Soumya Swaminathan, mwanasayansi wa shirika la Afya Duniani (WHO), alimwambia mwandishi wa Newsday Swahili
Wataalamu wanaonya kuwa watu wasitegemee kupata chanjo sokoni hivi karibuni.
David Nabbaro, Mkurugenzi wa afya katika chuo cha Imperial College, London, anasema wanadamu wataishi na hofu ya kutibu coronavirus ''kwa muda mrefu'' kwasababu hakuna hakikisho la kupatikana kwa chanjo mpaka sasa.
Nae Tim Lahey, mtafiti wa chanjo katika Chuo Kikuu cha matibabu cha Vermont, anaonya kwamba kuna "sababu kubwa ya kuwa na hofu chanjo ya virus vya corona huenda ikawa hatari kinga ya mwili pia".
Idadi ya watu waliambukizwa Covid-19 duniani tayari imepita milioni 2.5 huku zaidi ya vifo 177,000 vikiripotiwa.
Kutengeneza chanjo salama ambayo itasaidi kukabiliana na ugonjwa huo hatari , ni shughuli itakayochukua muda- kwa sababu itahitaji kufanyiwa uchunguzi wa kina wa kemikali na baolojia kabla itolewe rasmi. " akini tuna matumaini kwamba chanjo salama itapatikana katika muda wa miaka miwili au kabla ya muda huo kutimia," anasema Bw. Poonawalla.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Umoja wa Ulaya hatimaye wakubaliana kuufufua uchumi wao

Urusi kuisadia Uganda kujenga uwezo wake wa nyuklia, ni mataifa gani ya Afrika yanatumia nishati ya nyuklia na kwanini?