Jaji wa Mahakama ya Juu Marekani Ruth Ginsburg afariki

Jaji wa Mahakama ya Juu ya Marekani Ruth Bader Ginsburg, mpiganiaji wa haki za wanawake ambaye alikuwa jaji wa pili mwanamake katika mahakama hiyo, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 87
Kifo chake ambacho kimetokea wiki sita tu kabla ya Uchaguzi wa Rais huenda kikaanzisha mapambano makali ya kisiasa kuhusu kama Rais Donald Trump anapaswa kumteuwa, na baraza la Seneti linalodhibitiwa na Warepublican liidhinishe, mrithi wake, au kama kiti hicho kibaki wazi hadi baada ya kujulikana matokeo ya kinyang'anyiro chake dhidi ya Mdemocrat Joe Biden. Ginsburg ni Mliberali alijetambulika kwa kutetea haki za wanawake na jamii za walio wachache.
Kiongozi wa Maseneta wa Republican Mitch McConnell amesema Seneti itapiga kura ya kuidhinisha au kupinga jaji atakayependekezwa na Trump kumrithi Ginsburg, hata ingawa ni mwaka wa uchaguzi. 
Trump amemuita Ginsburg "mwanamke wa ajabu" na hakutaja kuhusu kujaza kiti chake kilichobaki wazi katika Mahakama ya Juu wakati akizungumza na wanahabari baada ya mkutano wa hadhara mjini Bemidji, Minnesota.
Biden alisema mshindi wa uchaguzi wa Novemba anapaswa kumchagua mrithi wa Ginsburg. "Hakuna shaka -- acha niwe wazi -- kwamba wapiga kura wanapaswa kumchagua rais naye rais anapaswa kumchagua jaji atakayeidhinishwa na Seneti," Biden aliwaambia wanahabari baada ya kurejea katika mji wake wa nyumbani wa Wilmington, Delaware, akitokea kampeni za Minnesota.
Siku chache kabla ya kifo chake, Ginsburg alimwambia mjukuu wake wa kike Clara Spera, kuwa matamanio yake makubwa ni kuwa nafasi yake haitajazwa hadi pale rais mpya atakapoapishwa. Hayo ni kwa mujibu wa radio ya umma nchini Marekani ya NPR
Jaji Mkuu John Roberts aliomboleza kifo cha Ginsburg. "Taifa letu limempoteza mwanasheria wa hadhi ya kihistoria. Sisi katika Mahakama ya Juu tumempoteza mwenzetu aliyependwa. Leo tunaomboleza, lakini na imani kuwa vizazi vya usoni vitamkumbuka Ruth Bader Ginsburg kama tulivyomfahamu -- mpiganiaji imara na asiyechoka wa sheria."
Ginsburg alitangaza Julai mwaka huu kuwa anafanyiwa matibabu kwenye ini lake, ikiwa ni mapambano yake kadhaa ya karibuni na ugonjwa wa saratani.
Follow us on Facebook
Follow us on Instagram
Follow us on Twitter
Subscribe our YouTube channel

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Umoja wa Ulaya hatimaye wakubaliana kuufufua uchumi wao

Urusi kuisadia Uganda kujenga uwezo wake wa nyuklia, ni mataifa gani ya Afrika yanatumia nishati ya nyuklia na kwanini?